Mkazi wa Kijiji cha Bugolola
wilayani Ukerewe mkoani Mwanza, John Chibuga (31) amehukumiwa kifungo cha miaka
30 jela baada ya kutiwa hatiani kwa unyang'anyi wa kutumia silaha.
Hukumu hiyo imetolewa jana
Februari 22.2024 na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa
Mahakama ya wilaya ya Ukerewe, Lucas Nyahega ambapo amesema kupitia
ushahidi uliotolewa mahakamani hapo, Mahakama imejiridhisha pasi na shaka
kwamba mshtakiwa ametenda kosa hilo na hivyo inamhukumu miaka 30 jela.
Awali, akisoma shtaka hilo,
Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Aidan Nziku alisema mshtakiwa alitenda kosa
hilo tarehe 15.12.2023 muda wa saa 14:00 mchana katika kijiji cha Kakerege
wilaya ya Ukerewe kwa kumvamia Mdala Mangu ( 34) akiwa Nyumbani kwake na
kumkata na panga sehemu mbalimbali ya mwili wake kisha kuiba simu ya mkononi na
kukimbia kinyume na kifungu namba 287A cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu sura 16
toleo la mwaka 2022.
Hata hivyo, mshitakiwa
alipopewa nafasi ya kujitetea ili apunguziwe adhabu kutokana na shitaka
linalomkabili,aliomba mahakama impunguzia adhabu kwa sababu alikuwa hana pesa
ya kujikimu baada ya kutoka gerezani ndio akaamua kwenda kupora.
Aidha, Mwendesha mashtaka
aliiambia mahakama kuwa mshitakiwa ni
mtenda kosa wa mara ya pili na aliachiliwa huru kwa msamaha wa Mhe. Rais tarehe
09.12.2023 kwa kosa la Kuvunja Duka Usiku na kuiba ambapo alitiwa hatiani na
mahakama ya Mwanzo Nansio na tarehe
15.12.2023 akarudia kutenda kosa.
Ili iwe fundisho kwake na
onyo kwa jamii hususani wafungwa wanaoachiwa huru kwa msamaha wa Mheshimiwa
Rais mwendesha mashtaka ameiomba mahakama hiyo itoe adhabu kali.
Kutoka Dawati la Habari Polisi Mwanza
By Pascal Kadushi
