WATUHUMIWA 115 MBARONI KWA MAKOSA YA WIZI,UVUVI HARAMU...MWANZA


Tarehe 15.01.2025, Jeshi la polisi Mwanza lilianza misako na doria ndani ya ziwa Victoria katika visiwa vya Yozu, Nyamango, Soswa na maeneo ya Kanyala na Mbugani kata ya Bulyaheke, Halmashauri ya Buchosa, baada ya kupata taarifa kutoka kwa wananchi kuwa kuna baadhi ya wahalifu wanasumbua katika maeneo hayo ya visiwa na fukwe. Kupitia misako hiyo tumefanikiwa kukamata watuhumiwa 42 kwa tuhuma za wizi wa samaki ziwani (Uhengaji), watuhumiwa 19 kwa tuhuma za kuishi nchini bila kibali, watuhumiwa 12 kwa tuhuma za kujihusisha na vitendo vya kihalifu, watuhumiwa 3 kwa kupatikana na nyavu haramu aina ya Timba, watuhumiwa 2 kwa kupatikana na Bhangi, watuhumiwa 16 kwa kujipatia kipato kwa njia ya ukahaba, watuhumiwa 3 kwa kukiuka masharti ya leseni ya biashara, watuhumiwa 12 kwa tuhuma za kucheza kamali, watuhumiwa 4 kwa kujeruhi, mtuhumiwa 1 kwa kupatikana na pombe ya moshi na mtuhumiwa 1 kwa tuhuma ya kumtaja mtu mchawi.




Lengo la misako na doria hizo ni kuzuia, kukamata na kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wa makosa mbalimbali tuliokuwa tunawasaka baada ya kupata taarifa zao za uhalifu kupitia mikutano ya hadhara ya ushirikishwaji jamii ambayo tumekuwa tukiifanya katika maeneo mbalimbali ikiwemo visiwa vya Ikulu, Chemagati, Chembaya, Zilagula, Mchangani, Ntama, Soswa, Nyamango, Yozu, Nyanzune, Bihira, Ito na mialo ya Kijiweni, Itabagumba, Kaunda na Kanyala. Mikutano ya ushirikishwaji wa jamii ililenga kuwapa wananchi elimu ya uvuvi salama, mazingira salama, ulinzi jirani na uundaji wa vikundi vya ulinzi shirikishi kupitia viongozi wa vitongoji, vijiji na kata.


Aidha, tumekamata vielelezo mbalimbali ikiwemo mitumbwi 6 isiyokuwa na namba za usajili ambayo inatumika kufanya wizi wa mazao ya uvuvi, mashine moja ya kuendeshea Boti, nyavu haramu vipande 1,500 aina ya timba (Mono filaments), Bhangi kilogramu 5 na pombe haramu ya moshi lita 30. Sambamba na hayo Jeshi la polisi linaendelea na hatua mbalimbali za kiuchunguzi dhidi ya uhalifu na wahalifu na mara zitakapokamilika, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watuhumiwa wote ikiwemo kuwafikisha mahakamani. Miongoni mwa watuhumiwa hao 115, watuhumiwa 31 wamefikishwa mahakamani ambapo watuhumiwa 11 wamehukumiwa kwenda jela miezi 12 baada ya kupatikana na hatia ya kujihusisha na ukahaba na watuhumiwa 20 kesi zao zinaendelea na zipo katika hatua mbalimbali, watuhumiwa wengine 81 watafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika


Operesheni hii ni endelevu na tutahakikisha tunafika visiwa vyote vya mkoa wa Mwanza, hivyo Jeshi la polisi mkoa Mwanza linatoa wito kwa wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada za kiusalama zinazofanywa na Jeshi la polisi ili kudumisha amani na usalama. Pia, tunawaomba wananchi kuendelea kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao



Post a Comment (0)
Previous Post Next Post