Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza limezindua kampeni ya wiki moja ya ukaguzi wa magari yanayotoa huduma za usafirishaji wa wanafunzi katika shule za Umma na binafsi Jijini humo kwa kuzingatia maeneo saba kwenye gari husika.
Aidha, Kamanda Mutafungwa amemuagiza Mkuu wa Kikosi cha usalama barabarani Mkoa wa Mwanza kuhakikisha wakaguzi wa magari hayo wanakuwa na vifaa vinavyohusika ili kuhakikisha kila gari linakaguliwa kwa kuzingatia vigezo na maelekezo aliyotoa.
Kamanda Mutafungwa amebainisha kuwa ukaguzi wa magari ya shule zote zilizoko katika wilaya ya Nyamagana na Ilemela utafanyika katika eneo la maegesho ‘gereji’ iliyopo nyuma ya Stendi ya Nyamhongolo wilayani Ilemela huku wilaya nyingine wakitakiwa kupeleka magari yao katika Vituo vya Polisi katika wilaya husika kabla shule hazijafunguliwa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani (RTO) Mkoani humo, Mrakibu wa Polisi (SP) Sunday Ibrahim amesema tayari magari zaidi ya 50 yamefikishwa katika gereji hiyo kwa ajili ya ukaguzi ambao ni bure; pia, amesisitiza kutembelea shule zote kwa ajili ya kubaini watakaokaidi zoezi hilo.
Akizungumza kwa niaba ya wamiliki wa shule, Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wamiliki wa Shule binafsi mkoani humo, Ezekiel Molel amewataka wenye magari kupeleka magari yao yakaguliwa huku akiahidi kutofumbia macho wale watakaokwepa ukaguzi huo muhimu.
Na Pascal kadushi




